Monday, July 1, 2013

MASHAIRI



--------------------------------------------------------------------------------

• Fasihi • Ushairi • Uchambuzi wa Mashairi
--------------------------------------------------------------------------------

Yafuatayo ni mambo muhimu unayohitajika kuzingatia kila unapochambua shairi.

Muundo/Umbo la shairi
Uhuru wa Mshairi
Maudhui
Dhamira
Mtindo wa / Mbinu za Lugha
Muundo/Umbo la Ushairi
Katika umbo wa shairi, tunaangazia jinsi shairi lilivyoundwa kwa kuangazia mizani, vina, mishororo n.k Aidha, ni muhimu kutaja aina na bahari za shairi zinazohusiana na kila sifa uliyoitaja.

Idadi ya mishororo katika kila ubeti - Tumia idadi ya mishororo kubainisha aina ya shairi hilo.
Kwa mfano: Shairi lina mishororo minne katika kile ubeti, kwa hivyo ni Tarbia
Idadi ya mizani katika kila mshororo na katika kila kipande cha mshororo.
Kwa mfano: Kila mshororo una mizani kumi na sita: nane katika utao na nane katika ukwapi.
Idadi ya vipande katika kila mshororo - Taja ikiwa shairi lina kipande kimoja, viwili, vitatu au vinne kisha utaje bahari yake.
Kituo, kiishio au kibwagizo - Ikiwa mstari wa mwisho umerudiwa rudiwa, basi shairi lina kibwagizo au kiitikio, la sivyo lina kiishio.
Vina - Zingatia vina vya kati na vya mwisho kutoka ubeti mmoja hadi mwingine. Kisha utaje ikiwa ni Mtiririko, Ukara au Ukaraguni
Uhuru wa Mshairi
Mshairi hafungwi na kanuni za kisarufi za lugha katika utunzi wa shairi. Anaweza kufanya makosa ya kisarufi kimakusudi ili shairi lizingatie umbo fulani. Zifuatazo ni njia mbalimbali ambazo mtunzi wa shairi anaweza kutumia kuonyesha uhuru wake.

Inkisari - kupunguza idadi ya silabi katika neno ili kusawazisha idadi ya mizani katika mshororo.
mfano: kubadilisha 'nimeona aliyenipenda' kuwa 'meona alenipenda'.
Mazda - kuongeza silabi katika neno ili kusawazisha idadi ya mizani katika mshororo.
mfano: afya ukijaliwa kuwa afiya ukijaliwa .
Tabdila - kubadilisha silabi ya mwisho ili kustawazisha urari wa vina katika kipande bila kuathiri mizani.
mfano: yahuzunisha dunia kuwa yahuzunisha duniya .
Kuboronga Sarufi -ni mbinu ya kupangua mpangilio wa maneno ili kuleta urari wa vina au mdundo wa ushairi.
mfano: siku hiyo ikifika kuwa ikifika hiyo siku .
Utohozi - Kuswahilisha Maneno - Wakati mwingine mshairi anaweza kubadilisha neno la lugha nyingine litamkike kwa Kiswahili ili kudumisha mdundo wa kishairi na pia kupata neno mwafaka litakalotimiza arudhi za kiushairi.
mfano: tukapata intaneti badala ya tukapata 'internet' ama mtandao wa tarakilishi.
Maudhui
Maudhui ni jumla ya ujumbe na mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika shairi fulani. Haya ni mambo yanayotajwa katika hadithi na yanaweza kujumuisha mawazo zaidi ya moja. Maudhui husaidia kujenga dhamira ya shairi.

Dhamira
Dhamira ni lengo, dhumuni au nia ya mtunzi wa shairi. Mtunzi wa shairi anaweza kuwa na kusudi la kutuonya, kututahadharisha au kutunasihi kuhusiana na jambo fulani.

Mtindo wa Lugha
Mtindo wa lugha hurejelea namna mbalimbali ambazo mshairi anatumia mbinu za lugha. Mshairi anaweza kutumia mbinu za lugha. kama vile: Tanakali za Sauti, Istiara, Takriri, Semi n.k
Angalia: Mbinu za Lugha katika Fasihi

No comments:

Post a Comment